Latest News 17 Nov 2022

News Images

MWAKIBETE AIPA MAJUKUMU MAZITO BODI MPYA YA MSCL

Serikali imeiagiza Bodi mpya ya Wakurugenzi wa Kampuni ya Huduma za Meli (MSCL), kusimamia kwa karibu taasisi hiyo ili miradi inayotekelezwa inakamilika kwa wakati na tija.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa bodi hiyo jijini Mwanza, Naibu Waziri wa Uchukuzi, Mhe. Atupele Mwakibete, amesema Serikali imewekeza zaidi ya bilioni 100 katika ujenzi na ukarabati wa meli katika maziwa yetu matatu (Ziwa Victoria, Ziwa Tanganyika na Ziwa Nyasa), hivyo haitavumilia kuona fedha hizo zikipotea kwa kukosa usimamizi mzuri.

“Serikali imetengea fedha zaidi ya shilingi bilioni 100 na fedha hizo zimehusisha ujenzi na ukarabati wa meli hivyo bodi mjipange kusimamia fedha hizo ili tuone matokeo ya uwekezaji wake", amesema Naibu Waziri huyo.

Aidha, Naibu Waziri Mwakibete ameiahidi menejimenti ya MSCL kuwa Serikali itaendelea kutatua changamoto mbalimbali zinazoikabili taasisi hiyo ikiwemo kuendelea kulipa mishahara mpaka pale itakapoweza kujiendesha na kupata faida.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya MSCL, Meja Jenerali Mst. John Mbungo, ameishukuru Serikali kwa kuteua wajumbe wenye utaalam kwenye maeneo mbalimbali ya sekta na nje ambao utawawezesha kusimamia kwa weledi taasisi hiyo ili ijiendeshe kibiashara na kuleta tija.

Mwenyekiti Meja Jenerali Mst. Mbungo amemuhakikishia Naibu Waziri Mwakibete kuwa bodi itawatumia wataalam walionao kuhakikisha miradi inakamilika kwa wakati na ubora.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa MSCL, Eng. Abel Gwanafyo, ameishukuru Serikali kwa kuendelea kuwekeza fedha ambazo zimeanza kuzaa matunda kwani meli tatu ilizokabidhiwa katika Ziwa Nyasa zimekuwa zikiongeza idadi na mizigo kila safari na hivyo kuinua kipato cha taasisi.

Naibu Waziri Mwakibete amezindua bodi ya MSCL yenye jumla ya wajumbe kumi (10) iliyochukua nafasi baada ya bodi iliyokuwepo kuvunjwa mwezi Disemba 2021.